Mmiliki wa Kampuni ya Ipp Dr Rejinald Mengi anatarajia kufungua kiwanda cha kutengeneza magari Tanzania (Made in Tanzania)

Mmiliki wa kampuni ya Ipp dr Rejinald Mengi anatarajia kufungua kiwanda cha kutengeneza magari Tanzania (Made in Tanzania)

       

Baada ya Dr Reginald Mengi kutangaza kujenga kiwanda cha kutengeneza simu kupitia kampuni yake ya IPP Touchmate, hivi karibuni Mengi ametangaza tena neema nyingine kwa watanzania kwa kutangaza kujenga kiwanda cha magari cha IPP Automobile Ltd. Kampuni hiyo ya IPP Automobile Ltd imeingia makubaliano na kampuni ya Youngsan Glonet Corporation ya Korea kwa ajili ya kuanzisha kiwanda hicho cha kuunda magari hapa nchini Tanzania. Makubaliano hayo yamefungua milango ya kuanza kwa kazi hiyo na inasemekana gari la kwanza litakuwa tayari kati ya mwezi Septemba na Oktoba hapo mwaka 2019.
 


Aidha Mwenyekiti wa kampuni za IPP, Dr Reginald Mengi amesema kuwa, uwekezaji wa Dola za marekani milioni 10 sawa na takribani shilingi za kitanzania bilioni 22 umefanyika katika kiwanda hicho kitakacho kuwa na makazi yake Kurasini jijini Dar es Salaam. Hata hivyo kwa mujibu wa Mengi kiwanda hicho kikianza kufanya kazi kitatoa ajira  kwa watanzania 500 huku ajira nyingine 500 zikiwa ni kwa watu watakao husika na uuzaji na usambazaji wa magari hayo. Hata hivyo, Mkurugenzi Mtendaji wa kampuni ya IPP Automobiles Ltd, Godfrey Bitesigirwe amesema, uagizaji rasmi wa vifaa vitakavyotumika kwa ajili ya uundaji wa magari hayo unatarajiwa kuanza mwezi Januari, mwaka 2019. Kwa sasa inasemekana kuwa magari yatakayo tengenezwa na kiwanda hicho cha IPP Automobiles Ltd yatakuwa ni kutoka kampuni za kutengeneza magari za Hyundai, Kia na Daewoo.

Maoni